DEKANIA YA ST.JOSEPH
DEKANIA YA UBUNGO
VIONGOZI WA DEKANIA YA KIBAHA
DEKANIA PETERS
DEKANIA YA ST. GASPAR
DEKANIA YA UKONGA
DEKANIA YA SEGEREA
DEKANIA YA KIGAMBONI
DEKANIA YA KILIMAHEWA
PAROKIA YA MWENGE
??
?HISTORIA YA PAROKIA YA MT. MAXIMILIA MARIA KOLBE MWENGE
1.0 UTANGULIZI
Hapo
mwanzo, katika kipindi cha miaka ya 1969 na 1985, Parokia ya Mwenge
ilizaliwa ndani ya jimbo Kuu la Dar es Salaam ikiwa mojawapo ya Parokia
kumi na moja (11) zilizofunguliwa chini ya uongozi wa Mwadhama Laurean
Kardinali Rugambwa. Katika kipindi hicho, Parokia ya Mwenge ilianza
mwezi Novemba 1973 kama Kigango chini ya usimamizi wa Parokia ya
Mwananyamala. Kwa muda wa miaka minane (Nov. 1973 – Mei 1981), Baraza la
Walei la Kigango liliwajibika kwa Halmashauri ya Parokia kwa mambo
yote. Mwezi Mei 1981 Baba Askofu Mwadhama Laurean Kardinali Rugambwa
alitoa idhini kwa Baraza la Kigango kuamua baadhi ya mambo na
kuyawasilisha moja kwa moja kwenye Baraza la Walei Jimbo. Ndani ya miaka
minne iliyofuata, Kigango kilipata hadhi ya kuwa Parokia mapema mwaka
1985.
Wakati Parokia ya Mwenge inazinduliwa mwaka huo 1985,
iliwekwa chini ya usimamizi wa Mtakatifu Maximilian Maria Kolbe ikiwa
kwa wakati huo ni Parokia ya ishirini na moja (21) katika Jimbo Kuu la
Dar es Salaam. Jina la msimamizi wa Parokia lilipendekezwa na Paroko wa
kwanza Mhe. Padre Zeno Zgudziak SDS kwa vile Mt. Maximilian Maria Kolbe
alikuwa ametangazwa rasmi tarehe 10 Oktoba, 1982 na Baba Mtakatifu Papa
Yohane Paulo wa Pili. Halmashauri Walei Parokia ilikubaliana na
pendekezo hilo na kulipitisha kwa kauli moja.
2.0 KUANZISHWA KWA KIGANGO NA HATIMAYE PAROKIA
2.1 Kupatikana kwa kiwanja
Historia
ya Mwenge yaweza kuchukuliwa kuwa ilianza mwaka 1973 pale ambapo
Wakatoliki waliokuwa wamejiunga na Chama cha Ushirika cha Ujenzi wa
Nyumba Mwenge (Mwenge Housing Co-operative Society Ltd.) walipoanza
kuhamia katika nyumba zao. Jumapili moja asubuhi mwaka 1973 baadhi ya
Wakristo hao wa Mwenge Kijijini walisimama kituoni, Barabara ya Bagamoyo
(sasa ni Ally Hassan Mwinyi) wakisubiri usafiri wa mabasi yaendayo
Kawe, Kariakoo, au Stesheni ili waweze kuwahi popote kwenye kanisa
kushiriki ibada ya Dominika. Bahati mbaya usafiri uliwatupa mkono siku
ile, nao kwa uchungu walirudi nyumbani.
Kwa bahati nzuri,
wakristo hao hawakukaa kimya kwani kutokana na matatizo kama hayo ya
mara kwa mara, kikundi cha Wakatoliki wakereketwa walikutana katika
nyumba ya Bwana Peter Masaiya hapo Mwenge Kijijini (Nyumba Na. 52/43)
ili kujadili masahibu yao. Kwa pamoja walikubaliana kutuma ujumbe wa
watu wawili kwenda kumwona Padre George Smith wa Parokia ya Mwananyamala
ili aweze kutatua matatizo ya Wakristo wa Mwenge. Ujumbe huo
ulishauriwa kuwasiliana pia na Mapadre wa Kawe na Chuo Kikuu wakati
wakisubiri kujua Mwenge itawekwa chini ya uongozi wa Parokia ipi, kati
ya Kawe, Chuo Kikuu na Mwananyamala. Ingawa juhudi za kwanza
zilishaonekana kwa kuja kwa Padre kutoka Chuo Kikuu na kuadhimisha Ibada
ya Misa chini ya Mkorosho, bado matatizo ya waamini hao yalibakia
palepale. Ilitokea siku moja, Sista Ursula Hopfensitz SDS ambaye alikuwa
akifundisha dini wanafunzi wa Kidato cha tano (V) na sita (VI) katika
shule ya Aga Khan (sasa Mzizima) kusikia shida ya Wakristo wa Mwenge
Kijijini, ambapo alimwomba mwanafunzi mmoja aitwaye Richard Nkwazi
kufuatana naye hadi Mwenge ili aonane na viongozi wa Kamati
iliyoteuliwa. Kwa pamoja walifanya majadiliano ya kutosha na Sista
Ursula akaahidi kurudi tena Mwenge akiwa na Padre wa Mwananyamala.
Baada
ya kujulikana Mwenge itakuwa chini ya Parokia ya Mwananyamala, Paroko
Msaidizi wa Mwananyamala Padre Adelhem Grab, OSB, akifuatana na Sista
Ursula Hopfensitz SDS walitembelea Mwenge tarehe 18 Novemba 1973 na
kukutana na baadhi ya wakristo na kuzungumzia matatizo ya kukosa huduma
za kiroho mahali hapo. Siku hiyo Padre Adelhem alisoma misa ya kwanza
Mwenge na wakristo wapatao 55 walihudhuria.
Baada ya misa hiyo,
Halmashauri ya kwanza ilikaa na Padre Adelhem Grab O.S.B. na kuchagua
Kamati ya watu wanane (8) chini ya Uenyekiti wa Bwana Peter Masaiya ili
isaidiane na Padre kutafuta kiwanja cha kujenga kibanda cha kusomea
misa na vilevile kusimamia na kuendeleza shughuli za dini katika eneo la
Mwenge. Tarehe 24 Novemba 1973, Wajumbe wa Halmashauri wakiwa pamoja na
Padre Adelhelm walijulishwa na kuonyeshwa eneo ambalo lilikwisha
kutengwa na serikali kwa ajili ya shughuli za kidini. Idhini hiyo iko
katika barua kumb. Na. LD/44/475/272/PJC ya tarehe 24 Januari 1972
kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo Mijini, aliyoandikiwa Askofu
Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam.
Kwa wakati huo, shughuli za
ibada ya misa na mafundisho ya dini zilikuwa zikifanywa nje chini ya
mkorosho kwenye ofisi ya Chama cha Ushirika cha Ujenzi wa Nyumba Mwenge
ambayo sasa ni ofisi ya CCM karibu na kituo cha mabasi ya Daladala
Mwenge. Padre Adelhelm alisifu sana moyo wa Wakristo wa Mwenge. Yeye
pamoja na Wakristo hao walikubaliana kujenga banda la ibada, na aliahidi
kutoa mabati na misumari kwa ujenzi huo.
Tarehe 19 Januari 1974,
Halmashauri iliandika barua kwa Katibu wa Chama cha Ushirika cha Ujenzi
wa Nyumba Mwenge, ikielezea nia ya Waamini kutaka kuanza ujenzi wa
kibanda cha muda cha kusalia ndani ya eneo hilo, ambapo ma maombi hayo
yalikubaliwa.
2.2 UJENZI WA KANISA LA MUDA
Hatua hii
iliyofikiwa ilikuwa muhimu sana katika majadiliano na kuwavuta Wakristo
wa Mwenge kuelekeza nguvu zao katika ujenzi wa kanisa. Ni kutokana na
sababu hii hata Askofu Mkuu wa Jimbo aliandikiwa barua tarehe 24 Novemba
1973 akiombwa kibali na msaada wa kujenga kanisa, ukumbi wa Parokia na
nyumba ya Mapadre. Uongozi wa Jimbo uliruhusu ijengwe “Parish Hall”
kwanza, ambayo ingelitumika kama kanisa na kutoa angalizo kwamba ujenzi
wa kanisa ungetegemea ongezeko la idadi ya Wakristo katika eneo la
Mwenge.
Hatua muhimu na ya kimaendeleo iliyochukuliwa ilikuwa
kujenga na kukamilisha kibanda cha kufanyia ibada Jumapili. Baada ya
uongozi wa Kijiji kuridhia ombi la Wakristo kuanzisha kigango cha
Mwenge, ujenzi wa banda la miti ulianza Januari 1974 kutokana na
michango yao ya hiari. Kiasi cha shilingi 366/= kilipatikana na pia
Padre Adelhelm alitoa msaada wa mabati, papi na misumari kama
alivyoahidi. Banda hilo lililokuwa la miti na kukandikwa kwa udongo
(matope) mwekundu lilikuwa na ukubwa wa meta 5 kwa meta 10. Hili ndilo
lililokuwa kanisa la muda la kwanza la Mwenge ambalo lilikamilika mapema
mwezi Aprili 1974. Hivyo, ibada za Juma Kuu zilifanyika ndani ya banda
hilo na pia ibada ya Pasaka ikafanyika humo tarehe 14 Aprili 1974. Siku
hiyo ya Pasaka ilikuwa ni sikukuu kubwa kwa Wakristo wa Mwenge kwani
watoto 16 walipokea Komunyo ya Kwanza.
Hatua muhimu ya pili
katika maendeleo ya Mwenge ilikuwa ni ujenzi wa ukumbi wa Parokia
(Parish Hall) ambao baada ya kukamilika ulianza kutumiwa na kuendelea
kutumika kama kanisa. Hatua hii ilizingatia ongezeko la Wakristo pamoja
na juhudi zao na pia agizo la awali la Jimbo la kujengwa kwa Parish
Hall. Ujenzi ulianza mwezi Mei 1974 na kukamilika Agosti 1974. Wafadhili
wakuu wa ujenzi huo walikuwa Shirika la Mapadre wa Benediktini
(Benedictine Fathers). Aidha, kwa msaada mkubwa wa Padre Adelhelm wa
Parokia ya Mwananyamala, zilipatikana mbao za kukalia, meza, makabati na
mapambo mengine ya ndani. Padre Adelhelm alisaidia pia kuwapatia
wafadhili waliotoa kengele, kinanda na vifaa vingine vya ibada. Ujenzi
wa ukumbi ulimalizika mwezi Agosti ambapo tarehe 15 Agosti 1974,
ulifunguliwa rasmi ikiwa ni Sikukuu ya Kupalizwa Bikira Maria Mbinguni,
Misa ya kwanza ilisomwa ndani ya ukumbi huu na Wakristo wakaanza
kuutumia kwa ajili ya adhimisho la misa na ibada nyingine.
Baada
ya kuhamia katika Parish Hall (wakati huo kanisa jipya), banda la miti
lilitumika kama Shule ya Msingi ya Mwenge, baadaye banda hilo likaja
kutumika kama Shule ya Chekechea (Kindergarten) pekee iliyokuwepo Mwenge
kwa wakati huo. Katika kipindi cha mwaka 1975 hadi 1977, idadi ya
Wakristo waliokuwa wanasali Mwenge ilizidi kuongezeka. Hii ilitokana na
familia nyingi kuhamia katika nyumba zao katika maeneo ya Kitalu Na. 43
(Mwenge Kijijini), Vitalu Na. 44, 46 na 47 Kijitonyama. Ongezeko hili
lilisababisha “kanisa jipya” kufurika Waamini hata ikabidi Paroko
aongeze idadi ya misa za Dominika kufikia mbili. Pia aliamua kuwa, Padre
kutoka Mwananyamala anayehusika na Mwenge, aitembelee mara tatu kwa
wiki katika siku za kawaida ili kuwahudumia Wakristo.
3.0 MABADILIKO YA UONGOZI PAROKIA YA MWANANYAMALA
Mwaka
1978, palitokea mabadiliko katika uongozi wa Parokia Mama ya Mt. Martin
De Porres, Mwananyamala. Mapadre wa Shirika la Mtakatifu Benedicto
(OSB-Wabenediktini) baada ya kumaliza mkataba wao Desemba 1977, waliamua
kwenda Kenya na nafasi yao kuchukuliwa na Shirika la Wamisionari wa
Afrika (White Fathers). Chini ya uongozi wao, kulihimizwa kuongeza
jitihada za kujitegemea kwa kuanzisha mfuko au akaunti maalumu ya
Parokia na kufanya maamuzi ya kujiletea maendeleo. Kwa mfano ujenzi wa
choo cha kudumu ulifanyika katika kipindi hiki na kusimamiwa na
Halmashauri ya Kigango. Choo kilianza kutumika rasmi mwaka 1979.
Maendeleo
ya kanisa la Mwenge yalizidi kushamiri. Eneo la kanisa lilizidi
kupanuliwa na sehemu mpya ikaombwa kuongezwa kwa ajili ya ujenzi wa
nyumba ya Masista. Kibali kilitolewa na Chama cha Ushirika cha Ujenzi wa
Nyumba Mwenge kwa barua Kumb. Na. RM/M/26/7/79 ya tarehe 26/7/1979.
Mwezi
Julai 1979 yalitokea tena mabadiliko ya uongozi wa Parokia ya
Mwananyamala, ambapo Mapadre wa Shirika la Wamisionari wa Afrika
walipelekwa kufungua Parokia mpya ya Manzese na nafasi yao ilichukuliwa
na Mapadre wa Shirika la Konsolata. Katika kipindi hicho, huduma za
kiroho ziliendelea vizuri na idadi ya watoto waliopata Sakramenti ya
Ubatizo, Ekaristi na Kipaimara iliongezeka mwaka hadi mwaka. Sakramenti
ya Kipaimara iliendelea kutolewa Parokiani Mwananyamala hadi mwaka 1980.
4.0 KUTOLEWA SAKRAMENTI YA KIPAIMARA KIGANGONI MWENGE, 1981
Baada
ya majadiliano ya muda mrefu baina ya Kigango cha Mwenge na Parokia
Mama ya Mwananyamala kuhusu utolewaji wa Sakramenti ya Kipaimara ambayo
muda wote ilikuwa inatolewa tu Mwananyamala, Mwenge iliomba watoto wa
Mwenge wapewe Kipaimara palepale Mwenge na Askofu alikubali. Hivyo,
Jumamosi tarehe 23 Mei 1981 Askofu alifika Mwenge kutoa Kipaimara jambo
ambalo lilishuhudiwa na Waamini wengi pamoja na wageni mbalimbali. Ili
kulipa Baraza la Kigango nguvu na madaraka zaidi katika kukabiliana na
shughuli zake na kutaka lijitegemee hususan katika kuendeleza Kigango,
baraza liliruhusiwa kuwa na mwakilishi Jimboni kuanzia mwezi Mei 1981.
5.0 KUPANULIWA KWA UKUMBI WA PAROKIA, 1982
Katika
miaka ya 1980, Kigango cha Mwenge kilizidi kukua na mahitaji yake
yakawa mengi zaidi. Hivyo Parish Hall ilipanuliwa mwaka 1982 na wakati
huohuo ofisi ya Paroko na sakristia ziliongezwa kwa gharama ya shilingi
140,000/=. Mnara wa kengele pia ulijengwa na kukamilika. Kwa kazi hizi,
kulibadili sura ya Parish Hall na kulifanya liwe na hadhi ya kanisa
dogo.
5.1 UJENZI WA NYUMBA YA MAPADRE, 1983
Tarehe 24
Julai 1979, uongozi wa Kigango ulituma maombi Ushirika wa Mwenge ya
kuongezewa eneo linalopakana na kiwanja cha kanisa kwa upande wa nyuma
ya Parish Hall. Tarehe 26 Julai 1979, ombi hilo liliridhiwa na uongozi
wa Chama cha Ushirika Mwenge. Ingawa barua ya maombi haikutaja matumizi
ya sehemu hiyo, shabaha kubwa ilikuwa itumike kujenga nyumba ya Masista.
Lakini awali ya yote katika kipindi cha mwaka 1980 – 81 mipango ya
kujenga nyumba ya Mapadre ilianza kuandaliwa na Jimbo. Hii ilikuwa hatua
ya mwanzo kwa Mwenge kuelekea kuwa Parokia. Katika miaka hiyo
ilikadiriwa kuwa ujenzi wa nyumba ungegharimu shilingi 800,000/= au
zaidi.
Kunako tarehe 2 Agosti 1981, Jimbo lilishapata shilingi
450,000/= na lilikuwa mbioni kupata kiasi kilichobaki ili ujenzi uanze.
Aidha Baraza la Walei lilianza kuchangisha fedha kutoka kwa Waamini na
Paroko wa Mwananyamala, Mhe. Padre Thomas alitoa nguo za mitumba za
kuuza ili kupata fedha zaidi kwa ajili ya ujenzi huo. Ilipofika tarehe 4
Oktoba 1981, Halmashauri ya Kigango ilielezwa kwamba Jimbo
lilishafungua Akaunti kwa ajili ya ujenzi wa nyumba ya Mapadre ambayo
ilikadiriwa kugharimu shilingi 1,000,000/=. Kutokana na makadirio hayo,
Wakristo waliombwa kuchangia walau asilimia kumi (10%) ya kiasi hicho,
sawa na shilingi 100,000/= ndani ya kipindi cha miezi sita.
Mwaka
1983 ujenzi wa nyumba ya Mapadre ulianza. Katika kipindi hiki kulikuwepo
na changamoto kubwa ya kutokuwepo na usimamizi wa karibu na wa kutosha,
na la pili na muhimu zaidi, ilikuwa bado kujulikana Shirika lipi
litapewa jukumu la kuongoza Mwenge. Suala hili lilikuwa bado mikononi
mwa Askofu Mkuu ambaye, alifanya juhudi kumpata Padre ambaye angeiongoza
Parokia tarajiwa.
6.0 KUTEULIWA KWA SHIRIKA LA MUNGU MWOKOZI
Baada
ya mawasiliano ya muda mrefu na Shirika la Wasalvatoriani, Mhe. Padre
Zeno Zgudziak SDS aliteuliwa kusimamia ujenzi wa nyumba ya Mapadre,
hivyo akafika Mwenge kufanya kazi hiyo. Kuanzia mwezi Januari 1985 Padre
Zeno Zgudziak SDS, alifanya kazi ya kusimamia ujenzi akisaidiawa na
Baraza la Kigango pamoja na Wakristo. Alipewa msaada mkubwa na Waamini
katika kukamilisha kazi ya ujenzi na mwezi Februari 1985, Padre Zeno
aliteuliwa kuwa Msimamizi wa Parokia tarajiwa ya Mwenge.
Mwezi Juni
1985, ujenzi wa nyumba ya Mapadre ulikamilika. Tarehe 16 Juni 1985 Mhe.
Padre Zeno Zguadziak SDS aliteuliwa rasmi na kutangazwa kuwa Kigango cha
Mwenge kimepata hadhi ya kuwa Parokia na kuwa yeye ndiye Paroko wa
kwanza wa Parokia mpya ya Mwenge. Tarehe hiyohiyo, Padre Zeno alihamia
kwenye nyumba ya Parokia, Mwenge.
6.1 KUJA KWA MASISTA WA SHIRIKA LA MISERIKORDIA (Masista wa Huruma)
Nyuma
ya jengo lililokuwa “Parish Hall” ambalo kwa muda mrefu (1974 – 1992)
lilitumika kama kanisa na hivi sasa ni shule ya Chekechea, kuna majengo
ya Shirika la Masista wa Misericordia wa Verona ambamo huishi Masista
Wamisionari na Masista wazalendo wa Shirika hilo. Tangu kipindi cha
miaka mingi Masista wa Shirika la Misericordia wa Tanzania walipenda
kuishi katika jumuiya za Dar es Salaam kwa lengo la kueneza Karama ya
Huruma. Pia katika kufundisha neno la Mungu na kushiriki katika shughuli
zote za Parokia.
Mwaka 1979 Masista walitoa ombi kwa Askofu Mkuu
wa Jimbo la Dar es Salaam Laurian Kardinali Rugambwa kuwapatia mahali
pa kukaa, ambapo aliridhia waishi katika Parokia ya Mwenge.
Katika
kipindi cha mwaka 1985, nyumba za kuishi Masista zilikuwa zikijengwa.
Tarehe 17 Desemba 1986 Masista wawili, Sista. Luisacarla Rossi na Sr. N.
Silvana Vettorello walihamia rasmi na kuanza maisha ya jumuiya. Baadae
walijiunga Sr. Mary John na Sr. Agnes Matonya. Kuanzia mwaka 1987
walianza kufundisha dini mashuleni na kujihusisha na vyama vya kitume,
hususan jumuiya ya Vijana Wakatoliki Wafanyakazi (VIWAWA) na pia
kuanzisha Shirika la Watoto la Kipapa (VIPAPA). Kuwepo kwa Masista hawa
kuliongeza ubora wa kazi za kitume, kwani manufaa mengi yalipatikana
kutokana na kuwafundisha wasichana na akina mama hasa kazi za kushona na
kazi nyingine za mikono zikiwemo za mapishi. Pamoja na kazi hizo,
Masista hawa hushughulika na kazi za kanisa kama vile mafundisho ya
watoto wa Komunio ya Kwanza, Kipaimara na kufundisha somo la dini katika
shule za msingi ndani ya Parokia.
Aidha, kwa miaka ya hivi
karibuni, mapema mwaka 1996, baada ya kupewa jengo la Ukumbi wa Parokia
(kanisa la zamani) walilifanyia ukarabati mkubwa kwa madhumuni ya
kujenga kituo cha watoto wadogo na kuanzisha shule ya chekechea kwa
watoto wenye umri wa miaka 4 hadi 6. Shule hiyo ya chekechea inajulikana
kama Bikira Maria Nyota ya Bahari. Mkataba kuhusu ujenzi na uendeshaji
wa kituo hicho katika Parokia ya Mwenge uliridhiwa tarehe 5 Septemba
1996 na Askofu Mkuu Mhashamu Polycarp Kardinali Pengo, Jimbo Kuu la Dar
es Salaam na Mama Mkuu wa Masista wa Misericodia, Kanda ya Tanzania.
7.0 UZINDUZI WA PAROKIA YA MT. MAXIMILIAN MARIA KOLBE, MWENGE
Tarehe
29 Septemba 1985, Parokia ya Mwenge ilizinduliwa rasmi na Mwadhama
Laurean Kardinali Rugambwa aliyekuwa askofu Mkuu wa Jimbo la Dar es
Salaam. Misa ya uzinduzi ilihudhuriwa na maelfu ya Wakristu
waliokadiriwa kufikia 1,500 wakiwemo viongozi wa serikali.
Kwa namna
Fulani kati ya Vigango vya Jimbo Kuu la Dar es Salaam vilivyobahatika
kupandishwa hadhi, Mwenge ilishika nafasi ya pekee. Kwanza maendeleo
yalikuwa ya haraka. Pili Wakristo walikuwa na ari kubwa sana kiasi
wakati mwingine Jimbo liliona kama vile linasukumwa. Lakini jimbo pia
liliitikia, kwani Mwenge ilipewa hadhi ya Parokia hata kabla ya
kutangazwa rasmi na Askofu Mkuu. Hii ilitokana haswa na ushirikiano
kati ya Baraza, Wakristu na Paroko Msaidizi wa Parokia ya Mwananyamala
Padre Aloisi Accossato I.M.C. ambaye kwa namna ya pekee alivutiwa sana
na taratibu za Mwenge na daima aliunga mkono maamuzi ya Baraza la
Kigango. Mwenge hata hivyo sio wakati wote walionekana kuwa wazuri ila
wakati fulani wajumbe wa Baraza la Mwenge waliitwa wakorofi kwa ile ari
yao ya kutaka uamuzi fulani ufanyike haraka na mara nyingine bila
kusubiri maoni ya Baraza la Parokia Mama.
Wakati Mwenge
inazinduliwa kuwa Parokia mwaka 1985, ilikisiwa kuwa na Waamini wapatao
10,000 au zaidi wakiwa wanaishi katika maeneo yafuatayo: Kijitonyama
yenye Mwenge Kijijini (Kitalu Na. 43); Vitalu Na. 44, 46 na 47; Mwenge
Jeshini, Mlalakuwa na Mikocheni. Maeneo matano ya Sinza (Vitalu A mpaka
E) ambayo sasa ni Parokia; na eneo la Makumbusho Kijijini na Makumbusho
Flats yaliongezwa baadae. Kwa mujibu wa taarifa ya mwaka 1994,
inayozingatia kuongezwa kwa maeneo hayo mawili hapo juu, idadi ya
Waamini iliripotiwa kufikia 10,500. Tangu kuzinduliwa kwake, Parokia
iliendelea kustawi na idadi ya Waamini kuongezeka hadi Vigango vyake vya
Sinza na Mikocheni navyo vikakua na kupata hadhi ya Parokia mwaka 1997
Sinza na 2006 Mikocheni.
7.1 MWENGE PAROKIA CHANGA: 1985 – 1997
Katika
awamu ya miaka hii (1985 – 1997), Parokia ya Mwenge ilistawi
kiuchungaji na ikafanikiwa kupata vigango viwili. Kigango cha Sinza
kilichokabidhiwa rasmi kwa Parokia ya Mwenge tarehe 23 Oktoba 1985,
kiliendelezwa na hatimaye mwezi Desemba 1997 kikapata hadhi ya kuwa
Parokia, na cha pili ni Kigango cha Mikocheni. Aidha, mafanikio hayo
yaliweza kupatikana pamoja na mambo mengine ya kuonyesha jinsi Parokia
ilivyoshika kasi kubwa ya maendeleo katika kipindi hicho, yakiwemo
yafuatayo:
• Kujenga Kanisa jipya Mwenge ambalo lilibarikiwa tarehe 16 Agosti 1992;
• Kujenga Kanisa la Kigango cha Sinza lililozinduliwa rasmi tarehe 30 Aprili 1989;
• Kujenga nyumba ya Mapadre wa Mwenge na Sinza zenye gorofa moja;
• Kuanzisha na kuendeleza Kigango cha Mikocheni;
• Kupadrishwa kwa Shemasi Henry Mchamungu tarehe 24 Juni 1994 akiwa tunda la kwanza la Parokia ya Mwenge;
• Kupadrishwa kwa Shemasi Paul Njoka tarehe 5 Julai 1997 akiwa tunda la pili la Parokia;
• Upanuzi wa kiwanja cha Mwenge kwa kununua nyumba Na. 382/43, Agosti 1997;
• Ujensi wa Grotto la kwanza la Bikira Maria, ukingoni mwa Maximilian Square Mwenge;
•
Uinjilishaji kupitia Kwaya ya Mt. Cesilia Mwenge hasa kwa kanda za
Mwaka wa Bikira Maria (1987-1988) na ujio wa Baba Mtakatifu mwaka 1990
nk
8.0 UJENZI WA KANISA LA KUDUMU, MWENGE
Haja ya kuwa
na kanisa kubwa Mwenge, ilikuwa imeanza kuonekana hasa wakati Jimbo
lilipoamua kukifanya Kigango cha Mwenge kuwa Parokia kwa vile idadi ya
Wakristu ilikuwa inaongezeka kwa sababu watu walikuwa wanahamia maeneo
mapya ya Kijitonyama. Hivyo, katika kuipa Mwenge hadhi ya Parokia
ilibidi mipaka yake ya kuhudumia ipanuliwe kiparokia kwa kuongeza eneo
lote la Sinza (ambalo robo tatu yake lilikuwa chini ya Parokia ya
Manzese – Kanda ya Sinza), eneo la Mikocheni B (ambalo lilikuwa nusu
yake linahudumiwa na Parokia ya Kawe na nusu nyingine ikihudumiwa na
Parokia ya Mt. Petro Oysterbay).
Mahitaji ya Kanisa jipya
yalijionyesha wazi pia kanisani Mwenge katika idadi kubwa ya Waamini
waliokuwa wanahudhuria misa siku za Dominika mwezi Novemba 1985, Mwezi
Januari 1986 ilibidi ianzishwe misa ya nne ili kupunguza msongamano
katika misa zilizokuwepo. Wakati huohuo, Paroko alilazimika kuanzisha
Kigango kuhudumia Wakristo waliokuwa wanakaa eneo la Sinza, pamoja na
kwamba viongozi wa Jimbo walikuwa wamemtahadharisha Paroko kuhusu
upatikanaji wa Mapadre wa kuja Mwenge kumsaidia katika kutoa huduma za
kichungaji. Kuanzishwa kwa Kigango Sinza kulipunguza kwa kiasi kikubwa
msongamano kwenye misa katika kikanisa cha Mwenge. Hata hivyo msongamano
ulizidi kuongezeka na ufumbuzi wake haukuonekana dhahiri.
Mwezi
Juni 1986 Baraza la Walei la Parokia lilipitisha azimio la kuanzisha
mchango wa kudumu ili kuwe na mfuko wa kujenga kanisa jipya. Mchango huu
ulizinduliwa rasmi tarehe 17 Agosti 1986.
Wakristo wa maeneo yote
walifahamishwa uamuzi huu na mikakati ya kuwashirikisha katika ujenzi wa
kanisa jipya ulianzishwa rasmi kwa kuwachangisha kila familia katika
maeneo yao wanakoishi. Michoro ya Ramani ya kanisa jipya la Mwenge
ilianza kutayarishwa mapema na misaada ya fedha ilianza kutafutwa kutoka
kwa wafadhili mbalimbali ndani na nje ya nchi. Wa kwanza kupelekewa
ombi la msaada na ambao walikuwa wa kwanza kuitikia, walikuwa ni uongozi
wa Shirika la Wasalvatoriani ambao walitembelea Parokia ya Mwenge na
kujumuika na Waamini katika misa walioiadhimisha tarehe 29 Juni, 1986.
Aliyekuwa Balozi wa Papa hapa Tanzania wakati huo, Askofu Mkuu Vicenso
Moreni alikuwa wa kwanza kuombwa msaada wake wa hali na mali. Msaada wa
Balozi ulitolewa kwa njia ya ushauri wa aina ya kanisa ambalo linafaa
kwa hapa Mwenge na pia msaada wa fedha uliotolewa na Ofisi ya
“Propaganda Fide” huko Roma. Wafadhili wengine walioombwa msaada
walikuwa ni Shirika la “Missio” la Ujerumani Magh’aribi na Mashariki na
mashirika mengine ya kidini ya huko Ulaya na Amerika. Kutokana na
michango ya Wakristu pamoja na michango ya wafadhili kutoka nje ya nchi,
fedha iliyopatikana iliwezesha kuanza ujenzi katua ya kwanza. Ujenzi
ulianza rasmi Oktoba 1988 kwa awamu, ambapo awamu ya kwanza ilikuwa ni
kujenga nguzo na paa, kazi ambayo ilipewa Kampuni ya “Italfrem”. Ujenzi
uliendelea vizuri, na ilipofika mwisho wa mwaka 1988 nguzo zote na
kenchi pamoja na mashimo ya kusimamisha nguzo vilikuwa tayari
vimemiminwa.
Baada ya hatua ya kwanza kukamilika, ujenzi uliingia
awamu ya pili, kazi iliyopewa Kampuni ya “J.W. Ladwa”. Ujenzi
uliendelea vizuri, na michango ikawa inaendelea, kwa kubuni mbinu
mbalimbali za kupata fedha, ikiwa ni pamoja na kuandaa Matembezi ya
Hiari (Charity Walk), mnada wa vitu mbalimbali nk. Ilipofikia mwezi wa
Oktoba 1991 Kanisa likawa limekamilika.
Kanisa jipya lilizinduliwa
rasmi na kubarikiwa mwaka 1992 na Mwadhama Laurean Kardinali Rugambwa,
Askofu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam. Uzinduzi ulifanyika sanjari na
kusherehekea Sikukuu ya Somo wa Parokia Mt. Maximilian Kolbe. Miongoni
mwa wageni mashuhuri waliohudhuria sherehe hiyo, ni pamoja na aliyekuwa
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. John Samweli
Malechela (MB) akiwakilisha serikali, wageni kutoka Parokia mbalimbali,
viongozi na wageni wa madhehebu ya kiroho
9.0 VIGANGO VYA PAROKIA YA MWENGE
9.1 Kigango cha Sinza
Juhudi
za kuanzisha kigango Sinza zilianza mnamo mwaka 1981. Mwanzoni Wakristo
wa Sinza walikuwa wakisali kwenye makanisa ya Manzese, Chuo Kikuu na
hata Kanisa la Mt. Yosef. Wakati huo, Parokia ya Manzese, chini ya
uongozi wa Paroko, Padre Geraldo Chebanon ilikuwa ikimiliki Kanda zake
za Tandale Makuburi, Sinza, Ubungo National Housing nk. Ibada ya kwanza
katika eneo la Sinza ilifanyika mwaka 1981 kwenye shule ya msingi
Mugabe. Baada ya misa kulikuwa na kikao cha wakristo wa maeneo ya Sinza
ambao waliona umuhimu wa kuwa na kanisa katika eneo hilo. Kuanzia tarehe
3 Aprili 1982, hoja ya kiwanja cha kanisa Sinza ilijitokeza. Ilipofika
Oktoba 1983 mikakati ya ujenzi wa kanisa ilianza na jiwe la msingi
kuwekwa mwaka 1984. Wakati huo, bado uamuzi wa Parokia ipi itakuwa
msimamizi wa Kanisa la Sinza, kati ya Manzese na Mwenge haikuwa
imejulikana hadi tarehe 30 Septemba 1985, siku moja tu baada ya Mwenge
kuzinduliwa kuwa Parokia, ndio Waamini wa Sinza wakatangaziwa kuwa Sinza
itakuwa chini ya Parokia mpya ya Mwenge.
9.2 Kigango cha Mikocheni
Eneo
la Mikocheni lilionekana zaidi baada ya Mwenge kuwa Parokia mwaka 1985.
Watu wa eneo hili walikuwa wanasali Parokia za Kawe, Mt. Petro
Oysterbay, Upanga na Mt. Yosef. Uongozi wa Jimbo uliamua eneo la
Mikocheni liwe chini ya Parokia ya Mwenge na hadi kufikia tarehe 30 Mei
1998 idadi ya Waamini katika Kigango hicho cha Mt. Martha Mikocheni
ilizidi kuongezeka. Harakati za kutafuta kiwanja cha kujenga zilianza
kwa kasi, na Hati Na. 47558 ya Kiwanja iliyotolewa na Wizara ya Ardhi na
Maendeleo ya Makazi cha tarehe 26 Julai 1998 ilikabidhiwa uongozi wa
Kigango.
Baada ya kupata hati hiyo, kanisa la muda lilianza
kujengwa na huduma ya misa kutolewa kuanzia tarehe 25 Aprili 1999.
Juhudi za kukiendeleza Kigango hicho ziliendelea na ujenzi wa Kanisa la
kudumu ulianza tarehe 29 Julai 2002 na tarehe 26 Oktoba 2002 jiwe la
msingi liliwekwa na Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo. Hatua kwa hatua,
Ujenzi wa Ofisi (2003) na nyumba ya Mapadre (2005) ulifanyika, na baada
ya kukamilisha shughuli zote ilipofika tarehe 24 Juni 2006 siku ya kutoa
Sakramenti ya Kipaimara kwa watoto wa Kigango cha Mikocheni, Mwadhama
Polycarp Kardinali Pengo, wakati
10.0 UNUNUZI WA NYUMBA YA WAGENI, MWENGE
Mwezi
Agosti 1997, Parokia ilinunua nyumba Na. 382/43 ambayo inapakana na
kiwanja cha kanisa. Lengo la kununua nyumba hiyo, ilikuwa kupanua eneo
la kanisa ili kupata nafasi ya kutosha kuegesha magari ya waamini na pia
nafasi ya michezo na burudani kwa vijana. Nyumba hiyo ilinunuliwa kwa
mkopo wa shilingi 15,000,000/= ambazo waamini walichangia urejeshwaji
wake. Mwaka 2004 nyumba hiyo ilifanyiwa ukarabati mkubwa na ikaanza
kutumika kama nyumba ya wageni wa Parokia, hususan Mapadre, Mabruda,
Mafrateri nk. Kuanzia Mwezi Mei 2008, nyumba hiyo ilianza kutumiwa na
Mapadre wakazi kutokana na kuvunjwa kwa nyumba ya zamani.
10.1 UJENZI WA GROTTO JIPYA LA BIKIRA MARIA
Wazo
la kujenga Grotto la Bikira Maria lilijitokeza na mwaka 2005 ujenzi
ulianza rasmi na kukamilika 2006. Liliwekewa sanamu ya Bikira Maria,
iliyotolewa zawadi na Masista wa Misericordia. Grotto hilo lilizinduliwa
na kubarikiwa na Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo tarehe 10 Novemba
2007.
10.2 UTAFUTAJI NA UNUNUZI WA KIWANJA/ENEO MLALAKUWA
Baada
ya Kigango cha Mikocheni kupata hadhi ya Kigango tarehe 26 Novemba
2000, uongozi wa Parokia ya Mwenge ulijielekeza kwenye hoja iliyokuwa
imekaa kiporo kwa miaka mitatu tangu mwaka 1997. Wakati huo, pendekezo
lilitolewa na kukubaliwa na kikao cha Halmashauri Walei kwamba, Kanda ya
Mlalakuwa iandaliwe kuwa Kigango. Ili kufanikisha azma hiyo, Kamati
Tendaji ilikuwa imehimiza kwamba Waamini wa Kanda hiyo watafute sehemu
maalum ya kufanyia ibada kwenye eneo hilo. Hata hivyo juhudi hizi
hazikuzaa matunda. Suala hili lilisuasua na hata kusahaulika hadi mwaka
2003 lilipoibuka tena kwa taarifa iliyoletwa na uongozi wa Mlalakuwa
kuwa eneo la takriban robo tatu za ekari limepatikana na linauzwa kwa
kiasi cha shilingi 45,000,000/=. Uongozi wa Parokia ulienda kulikagua,
na kuridhia kuwa ni eneo zuri kwahali ya Mlalakuwa. Kiasi kilichotajwa
kilionekana kuwa changamoto kubwa kwa vile Parokia ilikuwa na miradi
miwili ya kujenga kwa wakati mmoja, kanisa na nyumba ya Mapadre
Mikocheni iliyokuwa inaendelea kwa nguvu za waamini wa Parokia ya
Mwenge.
Tarehe 10 Desemba 2003, uongozi ulifanya mawasiliano na
uongozi wa Jimbo kuomba msaada wa fedha na mkopo wenye masharti nafuu
kwa ajili ya kufanikisha ununuzi wa kiwanja hicho. Tarehe 29 Desemba
2003 na 6 Januari 2004 viongozi wa Jimbo walifika Mwenge na kujionea
eneo hilo na kuafiki linunuliwe. Katika mazungumzo yaliyofuata, Jimbo
lilikubali kutoa mkopo wa shilingi 20,000,000/= ili mradi fedha hiyo
irudishwe kabla ya tarehe 30 Aprili 2005 na wakati huohuo ziongezwe
jitihada za kutafuta tofauti iliyobaki ya shilingi 25,000,000/=
kukamilisha jumla ya shilingi 45,000,000/= zilizohitajika na muuzaji.
Kwa kuzingatia majukumu yaliyokuwepo, pamoja na Jimbo kujitolea kiwango
hicho,bado waamini wa Mwenge hawangaliweza, na hivyo kulazimika
kuahirisha zoezi hilo hadi hapo majukumu ya Mikocheni yatakapomalizika.
Katika
kikao cha Halmashauri Walei kilichofanyika tarehe 6 Aprili 2008
ilitolewa taarifa kuwa kiasi cha shilingi 2,000,000/= ndizo zilikuwa
zimekusanywa. Aidha, gharama za viwanja ziliendelea kupanda hadi eneo
husika kufikia shilingi 300,000,000/- mwaka 2009.
10.3 UJENZI WA NYUMBA MPYA YA MAPADRE:
Kazi
ya ujenzi wa nyumba mpya ya Mapadre ilianza kwa kufanya maandalizi ya
awali kwa kupata michoro inayokidhi, pamoja na kibali cha ujenzi Na.
004947 kilichotolewa tarehe 10 Desemba 2007. Wakati huo waamini walianza
kuchangia juhudi za ujenzi. Tarehe 12 Agosti 2007, wafadhili wa ndani
walikutana na kuanzisha rasmi mfuko wa ujenzi kwa kufanya uchangiaji
(Fund Raising) uliofana kwa kiasi kikubwa. Kutokana na juhudi hizo hadi
kufika Aprili 2008, kiasi cha 30,000,000 taslimu zilikuwa
zimeshapatikana. Ujenzi ulianza rasmi tarehe 1 Mei 2008 kwa kumkabidhi
mkandarasi M/S Eagle Building Contractors ambaye alifanya kazi hiyo
chini ya usimamizi wa kamati teule. Katka kutekeleza mradi huu, jengo la
zamani lilivunjwa ili kupisha ujenzi wa nyumba mpya. Mkandarasi alianza
kuvunja nyumba ya zamani kati ya tarehe 2 na 24 Mei 2008. Kazi ya
kuchimba msingi ilianza rasmi 2 Juni 2008, na kumalizika tarehe 12 Juni
2008. Hadi kufikia tarehe 31 Agosti 2009 ilikuwa imekamilika tayari kwa
Mapadre kuhamia. Nyumba ilibarikiwa na kuzinduliwa rasmi tarehe 6
Septemba 2009 na Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Askofu Mkuu wa Jimbo
Kuu la Dar es Salaam. Uzinduzi wa nyumba ulitanguliwa na n ibada
maalumu ya misa ya shukrani iliyoongozwa na Mwadhama, ambapo pia
alibariki kengele ya umeme inayogonga kwa kutumia mtambo wa kisasa
(automatic).
10. 4 KUSIMIKA SANAMU YA MT. MAXIMILIAN MARIA KOLBE.
Suala
la kupata na kusimika sanamu lilianza kwa juhudi zilizofanywa na
Paroko, Padre Christopher Luoga, SDS pamoja na Paroko Msaidizi Padre
Stanslaus Goral SDS, kwa msaada wa Mkuu wa Shirika la Wafransiskani wa
Conventuale, walioko Parokia ya Segerea. Kwa ujumla wake, Gharama ya
ununuzi, usafirishaji, kodi ya forodha na gharama nyingine kutoka Poland
hadi Dar es Salaam ilikuwa dola za Kimarekani 3,150 (USD 3,150). Sanamu
hiyo iliwasili Mwenge tarehe 27 Juni 2009 na kazi ya kuijengea ikaanza,
na hadi ilipokamilika, uzinduzi ulifanyika tarehe 20 Agosti 2009 kwa
Ibada ya iliongozwa na Mhashamu Methodius Kilaini, Askofu Msaidizi Jimbo
Kuu la Dar es Salaam. Katika ibada hiyo ya kusimika sanamu ya Mt.
Maximilian Maria Kolbe lilifanyika pia tukio jingine la kubariki msalaba
maalumu wa Jubilei ya Fedha ambao ulianza kuzungushwa na waamini katika
JNNK kikanda.
11.0 WATAWA WALIOONGOZA NA KUFANYA KAZI ZA KITUME MWENGE: 1985 - 2018
11.1 Maparoko na Maparoko Wasaidizi
Kama
ilivyodokezwa awali Parokia ya Mwenge ilianza Septemba 1985. Katika
kipindi chote hiki imekuwa ikiongozwa na kuhudumiwa na Mapadre
Wamisionari wa Shirika la Mungu Mwokozi (Wasalvatoriani) chini ya
Maparoko wa kudumu kwa vipindi mbalimbali na kwa mpangilio ufuatao:
MWAKA | JINA LA PAROKO | MPANGILIO | PAROKO MSAIDIZI | MWAKA | |
1 | Feb 1985 – Okt 1986 | Padre Zeno Zgudziak, SDS | Paroko wa Kwanza | Pd. Andrea Kielkowski, SDS | Jan 1986 – Jun 1986 Ago 1986 - Jan 1988 |
Ago 1985 – Des 1985 | Pd. Andrea Mysiura, SDS | Paroko wa Muda | Pd. Carol Gleason, SDS | Des 1988 – 1991 | |
2 | Jun 1986 – Sep 1991 | Padre Karol Szojda, SDS | Paroko wa Pili | Pd. Mathias Millanzi, SDS | Jan 1992 - Des1992 |
3 | Jan1993 – Mei 1994 | Pd. Mathias Millanzi, SDS | Paroko wa Tatu | Pd. Engelbert Hatlapa, SDS | 1991 - Ago 1993 |
4 | Ago1993 – Nov 1995 | Pd. James Aloys Weyker, SDS | Paroko wa Nne | Pd. Carol Gleason, SDS | Mei 1993 – 1995 |
5 | Nov1995 – Feb 1996 | Pd. Mieczyslaw Kijaczek, SDS | Paroko wa Tano | ||
6 | 1996 – 1998 | Pd. Krystian Golisz, SDS | Paroko wa Sita | Pd. Christopher Luoga, SDS Pd. Felix Kisaka, SDS Pd. Jude Massawe, SDS | Ago 1997 - 1998 Ago 1998 Juni 1998 – 1999 |
7 | 1999 – 2002 | Pd. Jude Massawe, SDS | Paroko wa Saba | Pd. Marian Hajzyk, SDS | Ago 2000 – Des 2001 |
8 | 2002 - Nov 2011 | Pd. Christopher Luoga, SDS | Paroko wa Nane | Pd. Stanslaus Goral, SDS | 2002 – |
9 | Jan 2012 – Ago 2012 | Pd. Vilanova Mahoo, SDS | Paroko wa Tisa | Pd Amon K. Swai, SDS Pd.AusonKamughisha, SDS Pd. Baraka Isuja, SDS | 2005 - 2006 2006 - Feb2008 Ago 2008 – Okt 2008 |
10 | Ago 2012 – Feb 2013 | Pd. Vincent Sabiiti, SDS | Paroko wa Kumi | ||
11 | Mar 2013 - | Eugine Reslinski | Paroko wa 11 | Pd. Sixbert Heri, SDS Pd. Felix Mkude, SDS Pd. Jeremia Msaki, SDS | 2013 2015 May 2018 |
11.2 WATAWA
Pamoja
na Paroko akiwa na wasaidizi wake, pia kumekuwepo na Watawa wa kike na
wa kiume kwa maana ya Masista na Mabruda ambao wamekuwa wakitoa huduma
mbalimbali ndani ya Parokia kama vile Katekesina kulea Vyama vya Kitume
nk. Hao ni pamoja na Mabruda wa Salvatoriani na Masista wa mashirika
yafuatayo:
• Masista wa Misericordia wa Verona (I.S.M.)
• Masista wa Shirika la Bibi Yetu wa Kilimanjaro (C.D.N.K.)
• Masista wa Shirika la Mt. Theresia (C.S.T.)
• Masista wa Shirika la Moyo Safiwa Maria, Mgolole Morogoro (C.I.M.C.)
• Shirika la Mabinti wa Maria (Daughters of Mary Immaculate-D.M.I.) Tabora
• Masista wa Shirika la Salvatoriani (SDS)
11.2.1 Masista wa Misericordia wa Verona (I.S.M.)
Masista
wa wa Shirika la Misericordia ndio waliokuwa wa kwanza kufanya kazi
katika Parokia ya Mwenge. Hili ni shirika la kimisionari la kimataifa
lenye makao yake makuu kule Verona nchini Italia. Kwa hapa Tanzania
makaoyake makuu yapo Dodoma. Sr. Luisacarla Rossi pamoja na Sr. N.
Silivana Vettorello ndio waliofika kwanza Parokiani tarehe 17 Desemba
1986. Baadaye walikuja masista wawili kujiunga nao; Sr.Mary John na Sr.
Agnes Matonya. Tangu wakati huo Masista wa Shirika hili wameendelea
kufanya kazi mbalimbali hapa Parokiani hadi hivi sasa. Hufundisha somo
la dini shule za msingi, hutoa mafundisho kwa watoto wanaojiandaa
kupokea Komunio ya Kwanza na Kipaimara, hulea vyama vya kitume vya
WAWATA, VIWAWA na VIPAPA, hushughulika na usafi na upambaji wa kanisa na
pia huendesha shule yao ya elimu ya awali ya Bikira Maria Nyota ya
Baharii iliyopo hapa Parokiani Mwenge.
11.2.2 Masista wa Shirika la Bibi Yetu wa Kilimanjaro (C.D.N.K.)
Masista
wa Shirika la Bibi Yetu wa Kilimanjaro (C.D.N.K.), walifika Mwenge
mwanzoni mwa mwaka 1993 na kununua nyumba Na. 375/43 katika eneo
laMwenge jirani sana na eneo la kanisa. Masista waanzilishi walioanza
katika nyumba hiyo ni Sr. Oresta Uisso, Sr. Agricolla Soka na Sr.
Innocensia. Mara tu walipofika walishiriki kwenye kazi za Parokia za
uinjilishaji ikiwemo ihamasishaji uanzishaji wa Legio Maria. Mwaka 1994,
Masista hawa walianza pia kufundisha somo la dini katika shule za
msingipamoja na kutoa mafundisho kwa watoto wanaojiandaa kupata Komunio
ya Kwanza na Kipaimara. Mpakasasa, Masista hawa bado wanaendelea na kazi
yao ya uinjilishaji pamoja na kusaidia kazi za liturjia na ibada
mbalimbali kanisani.
11.2.3 Masista wa Shirika la Mt. Theresia (C.S.T.)
Masista
wa Shirika hili ambao makao yao makuu yako Iringa ni kutoka shirika la
wamissionari wa Mtakatifu Teresia wa Mtoto Yesu (Teresia Mdogo)
Wateresina au Congregation Saint Teresia (CST), walifikaMwenge tangu
mwaka 1997. Mwezi Julai 2003 walihamia na kuanza kuishi katika nyumba
yao iliyoko Mikocheni A. Tangu wakati huo wamekuwa wakishughulika na
kazi za utume na umissionarikwa njia mbalimbali kama vile kufundisha
dini,uuguzi, ukatekista na maendeleo ya jamii (umaritane). Kabla ya
Kigango cha Mikocheni kuwa na ukumbi, Masista wa shirika hili la
Wateresina walikusanya watoto nyumbani na kuwafundishasala, michezo na
nyimbo Sunday School). Baadaye Parokia ya Mwenge iliwaomba rasmi wafanye
kazi yakufundisha vipindi vya somo la dini shuleni na Katekisimu kwa
watoto wa mafundisho ya Komunio ya Kwanza na kipaimara kwa Kigango cha
Mikocheni. Baada ya Mikochenikuwa Parokia, Masista hawa wameendelea
kutoa huduma katika Parokia ya Mt. Martha Mikochenina Mt. Maximilian
Kolbe Mwengechini ya usimamizi wa Mama Mkuu Sr. Florence Lutambi.
11.2.4 Masista wa Shirika la Moyo Safi wa Maria, Mgolole Morogoro (C.I.M.C.)
Masista
wa shirika hili walifika Mwenge tarehe 10 Januari 2003 wakiwa na lengo
kuu la kufanya kazi za utume ambazo ni kufundisha dini, kulea watoto
yatima, kusaidia wagonjwa,kutengeneza vifaa mbalimbali vya kanisa na
kufanya kazi za kichungaji kadiri ya mwongozo wa jimbo.
11.2.5 Masista wa Shirika la Mabinti wa Maria (Daughters of Mary Immaculate-D.M.I.) Tabora
Shirika
la Mabinti wa Maria wa Tabora (Daughters of Mary Immaculate – D.M.I.)
ni shirika lakitawa la kijimbolenye makao yake makuu Jimbo Katoliki la
Tabora. Mwanzoni kabisa Masista hawa, walifika Mwenge kutoa huduma
wakitokeakwenye nyumba yao iliyopo Msimbazi. Mwishoni mwa mwaka
1993walinunua nyumba huko Sinza Kitalu A ambapo masista wawili: Sr.
Maria Stella Mlangalla na Sr. Ana Mwacha walianza kuishi nakushiriki
kwenyekazi mbalmbal.Hatimaye mwaka 1995 Masistahawa walihamia kwenye
nyumba yao eneo la Sinza (Barabara ya Sam Nujoma) ambapo pia wamejenga
hospitali na shule ya chekechea. Chanzo cha kufika Parokia ya Mwenge
wakati huo, na sasa Parokia ya Sinza ni kutoa utume kwa jamii, hususan
kufundisha elimu dunia shule za msingi na dini shuleni.Wakati Sinza
ikiwa bado ni kigango chini ya Mwenge, Masista hawa walitoa huduma
katika maeneo ya kigango na tangu mwaka 1998 baada ya Sinza kuwa
Parokia, Masista hawa wameendelea kutoa huduma ya kufundisha shule za
msingi pamoja na kufundisha somo ladini katika shule zilizokondani ya
Parokia hiyo.
11.2.6 Masista wa Shirika la Salvatoriani (SDS)
Hawa
walifanya kazi kuanzia tarehe 26 Septemba 2003 hadi 2005. Waliombwa
kusaidia kufundisha dinikutokana na uhaba wa kuwapata walimu wa dini. Ni
Sr. Mechtides Nambunga SDS ndiye aliyeziba pengo la uhaba wa
Makatekista.
12.0 VIONGOZI HALMASHAURI WALEI
Kwa
kuzingatia kwamba uongozi ndani ya Parokia unajumuisha pia viongozi wa
Halmashauri Walei, ni vema kuitazama historia ya uongozi kadiri
ilivyobadilika katika vipindi mbalimbali vya uongozi. Kadiri ya Katiba
ya Halmashauri ya Walei Katoliki Tanzania (2001, 2003), uongozi ndani ya
Parokia huzingatia kuwepo kwa Halmashauri Walei Parokia na Kamati
Tendaji ya Parokia. Uongozi wa Halmashauri ulikuwa na utaratibu wa kuwa
na viongozi watano (5) wa Kamati Tendaji wa kuchaguliwa na Halmashauri
ya Parokia yenye wajumbe watatu (3) wa kuteuliwa na Paroko.
Katika
kipindi cha 1985 – 2010, uongozi wa Parokia uliimarishwa kwa
kuwashirikisha viongozi Halmashari Walei walioshika nyadhifa mbalimbali
kwa mujibu wa katiba na kuunda Kamati Tendaji za Parokia kwa vipindi
mbalimbali vinavyoonyeshwa. Muundo wa sasa wa Halmashauri Walei unaundwa
na viongozi watano (5) wa Kanda na Kamati Tendaji ya Parokia, ambao ni
Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti, Katibu, Katibu Msaidizi, Mweka Hazina na
Wenyeviti wa Vyama vya Kitume ngazi ya Parokia.
KAMATI TENDAJI YA HALMASHAURI WALEI KUANZIA MWAKA 1985 - 2018
MWAKA | KIONGOZI | WADHIFA | |
1 | 1985 –1986 | Helena Khamsini Peter Masaiya Simon Mnimbo Theodore Mahulu Athanasi Mapunda | Mwenyekiti Makamu Mwenyekiti Katibu Katibu Msaidizi Mweka Hazina |
1986 –1987 | Peter Masaiya Nathalia Mlengule Theodore Mahulu Elly Iwato Atanas Mapunda Joseph Dalotta | Mwenyekiti Makamu Mwenyekiti Katibu Katibu Msaidizi Mweka Hazina Mweka Hazina Msaidizi | |
2 | 1988 –1990 | Peter Masaiya Nathalia Mlengule Theodore Mahulu Elly Iwato Atanas Mapunda Joseph Dalotta | Mwenyekiti Makamu Mwenyekiti Katibu Katibu Msaidizi Mweka Hazina |
3 | 1991 –1993 | Peter Masaiya Gosbert Mbatina Theodore Mahulu Elly Iwato Atanas Mapunda Joseph Dalotta | Mwenyekiti Makamu Mwenyekiti Katibu Katibu Msaidizi Mweka Hazina |
4 | 1993 – 1995 | Peter Masaiya Gosbert Mbatina Theodore Mahulu Elly Iwato Atanas Mapunda Joseph Dalotta | Mwenyekiti Makamu Mwenyekiti Katibu Katibu Msaidizi Mweka Hazina Mweka Hazina Msaidizi |
5 | 1995 – 1997 | Gosbert Mbatina (RIP) Daniel M. Ndabi Edgar Kivenule (RIP) Juliana Mbogautwa Thomas Kadushi | Mwenyekiti Makamu Mwenyekiti Katibu Katibu Msaidizi Mweka Hazina |
6 | 1997 – 2001 | Helena Khamsini Daniel M. Ndabi Lazaro Mwakimbala Elly Iwato Justine Uiso | Mwenyekiti Makamu Mwenyekiti Katibu Katibu Msaidizi Mweka Hazina |
7 | 2001– 2003 | Daniel M. Ndabi Athanas Mapunda Severin Mbuya (RIP) Thomas Kadushi Joseph Mushumbusi | Mwenyekiti Makamu Mwenyekiti Katibu Katibu Msaidizi Mweka Hazina |
8 | 2004- 2006 | Athanas Mapunda Daniel Ndabi Severin Mbuya (RIP) Prosper Vedasto/Maria Mboye Joseph Mushumbusi | Mwenyekiti Makamu Mwenyekiti Katibu Katibu Msaidizi Mweka Hazina |
9 | 2007 – 2009 | Peter M. Ngowi Theresia Nzunda Maria Mwaka Mboye Solanus Ndunguru/Susan Mugurusi Aloisi Mwanga/Batilda Mnzava | Mwenyekiti Makamu Mwenyekiti Katibu Katibu Msaidizi Mweka Hazina |
10 | 2010 – 2013 | Peter M. Ngowi Solanus Ndunguru Maria Mwaka Mboye Prosper Vedasto Batilda Mnzava | Mwenyekiti Makamu Mwenyekiti Katibu Katibu Msaidizi Mweka Hazina |
11 | 2013 - 2015 | Linus A. Ngowi Anatoli Paulo Susan Mugurusi Francis Moshi Batilda Mnzava | Mwenyekiti Makamu Mwenyekiti Katibu Katibu Msaidizi Mweka Hazina |
12 | 2015 - | Linus A. Ngowi Anatoli Paulo Susan Mugurusi Francis Moshi Batilda Mnzava | Mwenyekiti Makamu Mwenyekiti Katibu Katibu Msaidizi Mweka Hazina |
12.1 KAMATI ZA PAROKIA
Parokiani
kuna Kamati Ndogondogo tano (5) za Kikatiba ambazo zinasimamia masuala
mbalimbali ya Parokia. Wenyeviti wa Kamati hizo, ni wajumbe wa Kamati
Tendaji ya Parokia. Kamati hizo ni:
KAMATI | MWENYEKITI | |
1 | Malezi na Familia | Mwenyekiti; Kamati Tendaji |
2 | Ibada na Liturjia | Makamu M/Kiti; Kamati Tendaji |
3 | Haki na Amani | Katibu; Kamati Tendaji |
4 | Elimu, Mafundisho ya Dini na Teolojia | Katibu Msaidizi; Kamati Tendaji |
5 | Mipango, Uchumi na Fedha | Mweka Hazina; Kamati Tendaji |
Aidha, pamoja na Kamati hizo, kuna Kamati nyingine ndogondogo vilevile ambazo siyo za kikatiba ambazo zimeundwa katika Parokia, ambazo ni:
- Kamati ya Ulinzi
- Kamati ya Afya
- Kamati ya Ardhi
12.2 UONGOZI WA KANDA
Viongozi
wa Kandani wajumbe wa Halmashauri Walei Parokia. Hadi mwaka 2000, kila
kanda ilikuwa inawakilishwa na Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti naKatibu.
Kuanzia mwaka 2001 uwakilishi katika Halmashauri uliongezeka kwa
kuongeza nafasi ya Mweka Hazina kwa kila Kanda. Katika kipindi cha mwaka
1985 – 1997 kulikuwepo jumla ya Kanda 16. Mwaka 1998, baada ya Sinza
kuwa Parokia, zilibaki Kanda 11. Kuanzia Januari 2007 baada ya Mikocheni
kuwa Parokia inayojitegemea, Parokia ya Mwenge sasa inazo jumlaya Kanda
nane (8) ambazo zote zina majina ya watakatifu.
12.3 UONGOZI WA JUMUIYA NDOGONDOGO ZA KIKRISTU (JNNK)
Juhudi
za kuanzisha JNNK katika Parokia ya Mwenge zilianza kuonekana mapema
hata kabla Mwenge haijawa Parokia. Mnamo tarehe 18 Desemba 1977, Jimbo
lilitoa mwongozo na semina juu ya umuhimu wa JNNK. Katika semina hiyo
wajumbe watatu kutoka Kigango cha Mwenge; Nd. Peter Masaiya
(Mwenyekiti); Nd. Paul Njoka (Mweka Hazina) na Ndugu Simon Nnimbo
(Katibu) walihudhuria. Baada ya hapo, Kigango kilifanikiwa kuanzisha
JNNK kuanzia Kanda moja hadi nyingine. Baadhi ya Wakristu kutoka Kanda
hizo ziliendelea kwa Wakristu kukutana na kuelezana mambo mbalimbali ya
kiimani na kimaendeleo hadi mwaka 1996 ambapo jumuiya ya kwanza ya Mt.
Yosef Mfanyakazi ilipozinduliwa tarehe 15 Agosti 1996 ndani ya eneo
lililojulikana kama “Mwenge Shuleni” katika Kanda ya 43 Mwenge Kijijini.
Uzinduzi ulifanywa na paroko wa mwenge, Mheshimiwa Padre Krystian
Golisz SDS, katka sherehe maalum iliyofanyika nyumbani kwa mmoja wa
wanajumuiya hiyo.
Kuanzia mwaka 1997 juhudi Zaidi za kuendeleza
na kuzindua JNNK ndani ya Parokia ziliongezeka. Katika taarifa ya
utendaji ya mwaka 1997, iliazimiwa kwamba mwaka 1998 uongozi wa maeneo
ya Kanda ungeimarishwa zaidi ili ndani ya kila Kanda maeneo yapewe
majina ya Watakatifu badala ya majina ya “kienyeji” yaliyokuwa
yakitumika. Halmashauri iliona kwamba hatua hiyo ingesaidia jitihada
zilizokuwa zinafanywa na uongozi wa Parokia kuanzisha rasmi JNNK. Hata
hivyo, kulingana na Katiba ya Halmashauri Walei Katoliki Tanzania
(marekebisho ya pili) uundaji rasmi wa JNNK ulifanyika na kukamilika
mwezi Novemba 1998, kwa kila jumuiya kufanya uchaguzi wa viongozi wanne,
wakiwemo: Mwenyekiti; Makamu Mwenyekiti; Katibu na Mweka Hazina.
Katikakikao cha Halmashauri Walei Parokia, kilichofanyika tarehe 18
Oktoba 1998, kilitoa maagizo kwamba uchaguzi wa viongozi hao ufanyike na
kukamilika ifikapo tarehe 28 Novemba 1998 ili kutoa nafasi ya kutosha
kwa ajili ya uzinduzi wa jumuiya Kikanda. Aidha kikao kilipokea na
kukubali ushauri wa Paroko Msaidizi, Padre Jude Massawe SDS, kwamba
majina ya Watakatifu somo wa jumuiya hizo yatokane na Watakatifu wa
miezi Kikanda. Mpango huo ulilenga kusaidia kuhakikisha kwamba majina ya
watakatifu katika jumuiya mbalimbali hayafanani na hivyo kuondoa utata
wa ugonganishi majina wakati wa kusoma misa ndani ya jumuiya husika.
Kutokana
na uamuzi huo, Kanda zilipewa uhuru wa kuchagua majina ya Watakatifu
somo kuendana na miezi, kati na Januari hadi Novemba kama ifuatavyo:
Makumbusho Flats (Januari); Kanda 47 (Februari); Makumbusho Kijijini
(Machi); Mikocheni Kanda A (Aprili); Mikocheeni Kanda B (Mei); Mwenge
Jeshini (Juni); Kanda 43 (Julai); Kanda 46 (Agosti); Kanda 44
(Septemba); Kanda ya Mlalakuwa (Oktoba); na Mikocheni Kanda STAMICO
(Novemba). Uzinduzi rasmi wa jumuiya nyingi ulifanyika mwezi Desemba1998
kwa upande wa kanda za Mikocheni. Mwaka wa 1999 (Januari na Februari),
wakati wa uongozi wa Padre Jude Massawe SDS zilizinduliwa JNNK upande wa
Kanda za Mwenge. Baada ya kuzinduliwa na kupewa majina ya somo
Watakatifu kwa mujibu wa miezi ya kalenda ya mwaka iliyotajwa hapo juu,
jumuiya zilianza kustawi kwa kasi kubwa.
Hadi tarehe 10 Novemba
2002 kulikuwepo jumla ya JNNK 114 ambazo zilikuwa hai. Hata hivyo,
wakati huo zilikuwa zinafanyika juhudi za kubaini maeneo ambayo
yalihitaji marekebisho kwa lengo la kuwa na dadi ya jumuiya zinazowiana
na mwongozo wa Jimbo wa kila jumuiya kuwa na familia katiya nane (8)
hadi kumi na tano (15) au ishirini (20). Hii ni kumwezesha kila
mwanajumuiya kuwa na uhusiano wa karibu zaidi na jirani yake.
Wanajumuiya hukutana kwa zamu, kila juma mara moja kwa mwanajumuiya
mwenzao ili kusali na kufanya ibada ya Biblia pamoja, kulingana na
mwongozo wa Parokia uliotolewa na Jimbo kwa kupitia mtaalamu wa JNNK.
Mtaalamu huyo, Sr. Maximilla, alifika Mwenge mwaka 1999 na 2000 kutoa
mafunzo kwa viongozi wote wa JNNK kuhusu jinsi ya kuanzisha, kuimarisha
na kuendesha ibada za jumuiya. Kabla ya kuanzishwa kwa JNNK uongozi wa
Halmashauri Walei ulijikita katika sehemu kuu nne: Ngazi ya Parokia,
Kigango, Kanda na Eneo/mtaa). Wakati huo, maeneo kadhaa ndiyo yaliyounda
Kanda. Vivyo hivyo, Kanda kadhaa ziliunda Kigango au Parokia. Madhalan
huko nyuma ilielezwa kwamba Kanda A – E, kwa maana ya Sinza Vitalu A - E
ndivyo viliunda Kigango cha Sinza ambacho hatimaye kikawa Parokia ya
Mt. Bikira Maria Mama wa Mwokozi, Sinza.
Katika taarifa ya mwaka
2003, Parokia ya Mwenge iliripotiwa kuwa na jumla ya JNNK 116
zilizokuwa hai. Mwaka 2006, baada ya Mikocheni kuwa Parokia, Parokia ya
Mwenge ilibakiwa na JNNK 94. Hali kadhalika, hadi sasa (2018) Parokia
ya Mwenhe ina Kanda nane (8) na kila Kanda ina wastani wa JNNK kati ya
10 na 16 isipokuwa Kanda moja ina Jumuiya tatu (3) na Kanda mbili zina
Jumuiya mbili (2) kila moja. Jumla ya Jumuiya zilizoko ni 79, huku idadi
ya familia/kaya kwenye kila Jumuiya ikiwa ni kati ya 8 - 15, ijapokuwa
nyingine zimekuwepo za familia kati ya 16 - 22.
KANDA | MAJINA YA SOMO WATAKATIFU wa KANDA | IDADI YA JUMUIYA | |
1 | Kanda 43 | Mt. Monica | 12 |
2 | Kanda 44 | Mt. Yosefu Mfanyakazi | 14 |
3 | Kanda 46 | Mt. Yohane Paulo | 16 |
4 | Kanda 47 | Mt. Yosefina Bakitha | 16 |
5 | Kanda ya Mlalakuwa | Mt. Antony wa Padua | 14 |
6 | Kanda ya Mwenge Jeshini | Wat. Petro na Paulo Mitume | 3 |
7 | Kanda ya Makumbusho Kijijini | Wat. Perpetua na Felisita | 2 |
8 | Kanda ya Makumbusho Flats | Mt. Ritha wa Kashia | 2 |
JUMLA YA KANDA NI 8 NA JUMUIYA NI 79 | 79 |
12.4 IDADI YA WAAMINI
Jumla ya Wakristu katika Parokia hutokana na taarifa zilizopokelewa Parokiani kutoka kwenye Kanda na JNNK ndani ya Kanda hizo. Takwimu hizo zitakuwa sahihi kwa kipindi hicho zinapopokelewa, lakini ieleweke kuwa daima kuna wahamiaji au wahamaji toka nje na ndani ya Parokia kwenda sehemu nyingine na wengine aghalabu hufariki dunia na wengine kuzaliwa.
Mwaka 1985 idadi ya waam